Makala ya Nguvu ya Hoja kwa KSB Jumapili Machi 28, 2010
na Ndugu Mwandawiro Mghanga

Usajili wa wapigaji kura unaendelea kote nchini. Shughuli hii itaendelea kwa siku arobaini na tano kisha itakamilika kwa kuongezewa muda wa mwezi mmoja. Haya yote yanajiri baada ya kuvunjiliwa mbali kwa Tume ya Kenya ya Kusimamia Uchaguzi na baadae kuundwa kwa Tume Huru ya Muda ya Kusimamia Uchaguzi. Siyo tu muda wa vipande vya kupiga kura umekwisha na hata kupitwa na wakati bali pia uchaguzi wa mwaka wa 2007 ulighubikwa na udanganyifu ambao ulitia taifa katika hali ya vita vya wenyewe kwa wenyewe. Hivyo basi kuwasajili wapiga kura upya kunakusudiwa kuleta uchaguzi huru na halali.
Ni haki na wajibu wa kila mwananchi kutumia fursa iliyopo kujisajili kuwa mpigaji kura. Kwani hakuna atakayekubaliwa kupiga kura bila kuwa na kipande kipya cha kupiga kura. Kujisajili kuwa mpigaji kura ni kujitayarisha kupiga kura za maoni kuhusu katiba mpya kutakakofanyika mwaka huu na vilevile kuwa mpigaji kura au mpigiwa kura kwa uchaguzi wa 2012 ambao wengi tunausibiri kwa hamu na ghamu. Kujisajili kuwa mpigaji kura ni uzalendo. Uzalendo ni kupenda nchi yako na kuwa tayari kuilinda na kuiendeleza kwa vyovyote vile. Ni kweli kwamba kura za mwaka wa 2007 zilisababisha maafa na mateso kwa wengi na hali hii bado haijarikebishwa maana wale waliyochochea, kuzatiti na kudhamini ghasia baada ya uchaguzi bado hawajachukuliwa hatua za kisheria.
Baadhi ya washukiwa bado wangali viongozi wa nchi hii. Aidha, wahanga wengi wa ghasia na vita hivyo bado wangali wakiteseka katika kambi za wakimbizi ndani ya nchi. Hali hii ni ya kuvunja moyo na inaweza kuwafanya wengi kukataa kujiandikisha kuwa wapigaji kura. Lakini kukataa kujiandikisha kuwa mpigaji kura kwa sababu yoyote ile ni kukosa busara. Katika maisha, matumaini ni uhai. Ukosefu wa matumaini ni mathalani kifo. Kukata shauri kukataa kupiga kura ati madhali unalalamikia jambo fulani ni ujinga kwani ni kupitia kwa kupiga kura ndipo unaweza kuathiri hali ya kusulihisha matatizo unayoyalalamikia.
Kuna wale ambao wanasema ati hawatajiandikisha kuwa wapigaji kura kabla ya kupatikana kwa katiba mpya. Ukweli ni kwamba katiba mpya itapatikana mwaka huu, hata ingawa haitaridhisha kila mtu, mimi nikiwemo. Bali katiba mpya si maisha mapya ingawa ikiwa bora inaweza kuwa ngazi ya kuwania maisha mapya. Hii inategemea siasa na harakati za kitabaka. Maana siasa na harakati za kitabaka ni mama wa mambo yote, yawe ya kisiasa, kiuchumi, kibiashara, kijamii, kitamaduni na ya kila hali. Ili kuwe na maisha mapya lazima Kenya ibadilike kisiasa, kijamii, kiuchumi, kitamaduni na kwa kila hali.
Aidha, siasa mbaya hazitatafsiri katiba mpya ili iboreshe maisha ya wengi. Tukumbuke kuwa wanasiasa watakaodhibiti nguvu za dola na serikali ndiyo vilevile watakaotafsiri na kutekeleza katiba mpya. Nao watatafsiri na kutekeleza katiba ili kutosheleza masilahi yao ya kiuchumi, kibiashara, kiitikadi na kitabaka. Viongozi wabaya wakiendelea kuongoza nchi hii wataendelea kutafsiri na kutekeleza katiba mpya kuongoza nchi yetu vibaya. Watatunga sheria za kuhakikisha mfumo wa ubepari na ukolonimamboleo unahifadhiwa na kuimarishwa nchini. Tukijisajili kuwa wapigaji kura kwa wingi na kuwa tayari kuzipiga vizuri basi tunaweza kusababisha mageuzi yatakayoleta mfumo wa haki na kimaendeleo nchini. Kulalamika tu bila kupiga kura hakutasaidia chochote maana ni sawa na kelele za chura ambazo hazimzuii ng’ombe kunywa maji.
Kupiga kura vizuri ni kuchagua viongozi wakweli, wazalendo, wateteaji wa uhuru na masilahi ya wengi na wenye uwezo na nia ya kuongoza nchi yetu kusuluhisha matatizo tilatila yaliyoko. Bali ikiwa tutaendelea kuwachagua viongozi kwa misingi ya kikabila, ujinga, kutojali ama kutokana na hongo, hali iliyopo nchini leo haitabadilika hata chembe hata tukiwa na katiba mpya. Maana siasa mbaya ni maisha mabaya. Isitoshe, katiba itakayokuja inalinda sana na mno mali ya binafsi. Na mali ya binafsi mara nyingi ni ngome ya kunyonya na kugandamiza tabaka la wengi, mafukara.
Hata hivyo kuna mambo mengi mazuri ndani ya katiba mpya inayoendelea kupigwa msasa sasa. Hata hivyo, mambo mazuri yaliyoko ndani ya katiba mpya yatatekelezwa tu ikiwa tutakuwa na serikali mpya na viongozi wapya watakaoleta uongozi na siasa mpya za kuzingatia masilahi ya kitaifa badala ya kibinafsi. Lazima tujisajili kuwa wapigaji kura ili kuondoa wafisadi, wanyonyaji na wadhalimu. Wala hakuna njia yoyote nyingine ya amani ya kuwapeleka mashujaa wa umma bungeni na uongozini isipokuwa kujitayarisha kupiga kura kwa uchaguzi ujao kwa kujisajili kuwa mpigaji kura sasa. Kumbuka kura ni silaha ya kupigania mageuzi na ukombozi.
Wakati shughuli ya kuwasajili wapigaji kura zinaendelea, tayari baadhi ya viongozi waliyopo na matajiri wameanza kutumia pesa kuathiri pahali mafukara watapigia kura. Wanawalipa na kuwahamisha mafukara kujisajili katika sehemu ambapo wanatarajia kupigania au kutetea viti katika uchaguzi ujao. Uhongaji katika uchaguzi ni hatari kwa amani na usalama nchini na vilevile ni pingamizi kwa kukua kwa demokrasi nchini. Tusikubali kujisajili kuwa wapigaji kura ili kuja kutumia kura zetu kupokea hongo katika uchaguzi. Kumbuka kiongozi atakayekupa hongo ili umpigie kura ni adui wako na wa maendeleo. Tahadhari naye!
Mwandawiro Mghanga, Barua pepe: mwandawiro2002(at)yahoo.com
Hey ndugu yangu, wathani tume hii mpya yakusimamia uchaguzi wa kirefaramu wata kwa huru kweli? Bado rais niyuleyule na sheria pia ni yaleyale, itakwa nadra sana tume hiyo ku endeleza kazi yake bila interfearence yoyote kutoka kwa serikali, Maana yake marahia waKenay hawa imani kwa serikali inayo endeleza mambo huko Kenya, lakini tuta waombea wa endese uchaguzi vizuri, hii ni yareferandamu na pia uchguzi kuu wa nchi.
Mugogo Bziegnew
Couldn’t read past the first sentence…, don’t know what happened but I’ve slowly tuned Kiswahili out of mind/brain after living in the US for so long and it’s a shame. It used to be so easy to read a novel or anything in Swahili. Reminds me I need to keep my culture alive because no matter where in the world I am, my true identity is a Kenyan.